ACT YASISITIZA MISWADA YA UCHAGUZI KUBORESHWA



Na Mwandishi wetu

CHAMA  cha ACT Wazalendo kimeendelea kuisisitiza Serikali kuhakikisha Miswada mitatu iliyopelekwa bungeni kuakisi maoni na mapendekezo ya wadau wa demokrasia nchini.

Miswada hiyo ni pamoja na Muswada wa Tume ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na mMdiwani, Muswada wa Sheria wa Vyama vya Siasa pamoja na Muswada wa gharama za Uchaguzi.

Kupitia hotuba ya Makamu Mwenyekiti wake, Doroth Semu (Bara) na Naibu Katibu Mkuu, Joran Bashange kwa nyakati tofauti viongozi hao waliwaambia wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Mkoa wa Morogoro na Tanga jana  kuwa chama hicho kitaendelea kusukuma uboreshaji wa miswada hiyo ili nchi iweze kuwa na uhuru wa kisiasa kama Taifa pamoja na kuhakikisha chaguzi zote za miaka ijayo zinakuwa huru, haki na zinazoaminika.

Doroth amesisitiza kwamba chaguzi zote zikiwamo za Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu ni lazima zisimamiwe na Tume ya Taifa ya Uchaguzi huku akipinga kifungu cha sheria kinachowaruhusu Wakurugenzi wa Halmashauri na majiji kusimamia chaguzi za aina zote ambapo amesema utafiti uliofanywa na chama hicho umebaini zaidi ya asilimia 50 ya wakurungezi hao ni makada na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi.

Aidha Doroth amesisitiza kuwa kupitia miswada hiyo, Sheria iweke kifungu mahsusi cha kuzuia mtu ambaye amewahi kushiriki kwenye siasa asiwe msimamizi wa Uchaguzi.

ACT Wazalendo kinapendekeza kuwepo kifungu cha sheria kuruhusu wajumbe wawili kwenye Tume ya Uchaguzi wanaotokana na vyama vya siasa vyenye uwakilishi bungeni kwa kuzingatia jinsia huku pia kikitaka sheria ya vyama vya siasa iwe na kifungu cha kuvibana na kuvielekeza vyama vyote kwenye nafasi za uamuzi kuwepo wanawake kwa kiwango fulani.



ACT Wazalendo pia inapendekeza kuwapo kwa  ruzuku kwa vyama vyote vya siasa kulingana na mapendekezo ya Kikosi kazi ili kusaidia kujiendesha na kuepuka matumizi ya fedha chafu.


Powered by Blogger.