ULINZI WA WANYAMAPORI WAIMARISHWA HIFADHI YA BURIGI






Na Mwandishi wetu,CHATO 

KAMISHNA wa Uhifadhi wa Shirika la hifadhi za Taifa (TANAPA) Juma Kuji amesema hifadhi ya Burigi Chato imeanza kutumia teknolojia za kisasa  kulinda hifadhi kwa  kutumia ndege zisizo na rubani(Drone).

Akizungumza leo Kamishna Kuji amesema wamejipanga kuongeza  doria katika hifadhi ili kuhakikisha wahalifu wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya Sheria na kuzuia kabisa hali ya uvamizi na ujangili katika eneo hilo.

 "Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) imejipanga kukomesha matukio ya ujangili na uvamizi wa Mifugo hifadhini ndio maana tumeanza  kutumia teknolojia za kisasa  kulinda hifadhi kwa  kutumia ndege zisizo na rubani  na nyingine ili kuhakikisha wahalifu wanakamatwa,"amesema.

Kamishna kuji ametoa wito kwa wananchi kuacha mara moja tabia za kuingia hifadhini na kufanya uhalifu ikiwemo kuingiza Mifugo katika maeneo hayo kwani lazima watakamatwa .

Naye  Mkuu wa     wa hifadhi hiyo, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi,Ismail Omar amesema Ulinzi wa hifadhi hiyo sasa umeimarika hali ambayo inasabisha utulivu wa Wanyamapori na Wanyamapori kuanza kuongezeka.

Omar amesema ,changamoto ambayo wanaendelea Kuidhibiti ni kuingizwa mifugo kutoka nchi jirani na baadhi ya viongozi wa vijiji wasio waadilifu .

"Tuna vijiji 38 vinavyozunguka hifadhi sasa baadhi ya maeneo kuna viongozi wanapokea wafugaji kutoka nchi jirani na kuingiza Mifugo hifadhini hasa katika maeneo ya milima na mabonde"amesema

Hata hivyo, amesema kutokana na matumizi ya Teknolojia za kisasa katika Ulinzi Mifugo imekuwa ikikamatwa na kufikishwa Mahakamani.

"Tunaomba viongozi wachache wa vijiji waache kuhujumu hifadhi na wajuwe lazima tutawakamata wao na Mifugo iliyoingizwa hifadhini"amesema.

Naye ,Afisa Uhifadhi Mkuu wa ldara ya Ulinzi,Deogratius Mwageni amesema   kukamatwa kwa Mifugo hiyo ni kutokana na kuimarika Ulinzi na akaonya baadhi ya viongozi wa vijiji kushirikiana na wahalifu kuingiza Mifugo hifadhini.

Mwanasheria na Kitengo cha uchunguzi na kuendeshaji kesi katika hifadhi ya Burigi -Chato, Emmanuel Zumba amesema wamekuwa na operesheni ya kukamata Mifugo hifadhini kuanzia Julai 2024 hadi sasa,wamekamata   Ng'ombe zaidi ya 1000 na wanakesi 165 na hadi sasa 74 zimetolewa uamuzi ambapo wameshinda.


Powered by Blogger.