WAFANYAKAZI STAMICO KWA PAMOJA WAUNGA MKONO MAGEUZI YA SHIRIKA KUELEKEA KUJITEGEMEA




Na Mwandishi wetu, DAR ES SALAAM 

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Dkt. Venance Mwasse amewataka Watumishi kuwa wabunifu na kufanya shughuli zao kwa tija ili kukuza uchumi wa Taifa hususan katika Mwaka wa Fedha 2024/25 ili kukuza uchumi kupitia sekta ya madini.

Dkt. Mwasse amebainisha hayo leo Julai 19, 2024 katika kikao kazi cha Watumishi wa STAMICO kilicholenga kufanya tathmini ya utekelezaji wa bajeti 2023/2024 na kuweka mikakati ya mafanikio kwa Mwaka wa Fedha 2024/25 jijini Dodoma

Ametumia kikao hicho kuwashukuru wanastamico kwa kuwa sehemu ya mageuzi haya sambamba na kuwakaribisha wafanyakazi wapya huku akiwaasa kwenda na kasi ya mageuzi ya shirika. 

Akitoa wasilisho la Fikra za Kibiashara katika kuendesha Shirika Mkufunzi kutoka Chuo Kikuu cha Mzumbe Dkt. Erenest Mwaswaliba amehimiza umuhimu wa kila mfanyakazi kubadilika na kuwa na fikra ya kijasiliamali wakati huu ambapo Shirika linaenda kujitegemea.



Amesema ili mageuzi hayo yaweze kuleta tija kwa Shirika ni lazima kubadilisha utamaduni wa utendaji kazi ambapo kila mfanyakazi anatakiwa kuwa sehemu ya mnyororo wa mabadiliko na mafanikio hayo bila kuweka vipingimamizi .

Aidha, amesema kujitegemea kwa Shirika kunahitaji wafanyakazi waliokuwa huru, kufanya kazi kibiashara na kuthamini wateja na wageni wote wanaokuja katika ofisi kuhitaji huduma.

Amesisitiza umuhimu wa kufanya kazi kwa kushirikiana badala ya kutegeana na kuacha idara nyingine ikiteketea kwa kigezo cha kutohusika na jukumu hilo, kwa kuwa ushirikiano ni silaha kuelekea mafanikio.

"Niwakumbushe kuwa meli inapotoboka haiwezi kuleta madhara eneo moja bali yote hivyo kila mtu anatakiwa kushiriki kutoa maji ili meli isizame." Amesema Dkt. Mwaswalubi


Kwa upande wake Meneja Mkuu wa Kampuni Tanzu ya Kuchimba Dhahabu STAMIGOLD Bw. Ally Ally ameshukuru kwa Uhusiano mzuri anaoupata kutoka STAMICO hususan kupitia biashara ya kemikali na Vilipuzi, Kiwanda cha kusafisha Dhahabu na uongozi bora na kuahidi kuendelea kufanya kazi bega kwa bega 

Naye, Afisa Uhusiano Mkuu Gabriel Nderumaki amewakumbusha wafanyakazi kuzingatia itifaki na adabu kazini ili kuleta uwajibikaji wa pamoja katika kutekeleza mageuzi.

Amehasisha wafanyakazi kujiamini na kuachana na hofu za migogoro kutakakosaidia kufanya maamuzi yenye tija kwa shirika yanayoendana na mageuzi.

Aidha, Mkurugezi wa Mipango Dkt. Venance Kasiki ametoa pongezi kwa uongozi wa STAMICO, kuandaa kikao na kutoa mafunzo ya kubadilisha fikra ili kuongeza uthubutu, utunzaji wa muda na kujali wateja 

STAMICO imefanya kikao maalum kwa wafanyakazi wake ili kubadilisha fikra za utendaji kazi ikiwa ni mwanzo wa utekelezaji wa mageuzi ya kihistoria yaliyofanyika na kuweka mkakati wa pamoja kuelekea nchi ya ahadi yenye maziwa na asali kuanzia Mwaka 2024/2025.

Powered by Blogger.