WIZARA YA NISHATI YAENDELEA KUTUMIA NISHATI SAFI EXPO KUTOA ELIMU KWA WANANCHI*

 *


Dar es Salaam


Wizara ya Nishati inaendelea kutoa elimu ya nishati safi ya kupikia kwa wananchi mbalimbali wanaoshiriki  Kongamano la Nishati Safi Expo 2026 linaloendelea jijini Dar es Salaam  hatua inayolenga kuimarisha afya za wananchi, kuhifadhi mazingira na kuboresha ustawi wa jamii.




Wananchi hao wanaelimishwa kuhusu aina mbalimbali za nishati safi ya kupikia ikiwemo gesi ya kupikia (LPG), gesi asilia, bayogesi, bayoethanoli, umeme pamoja na mkaa mbadala.


 Aidha, wanapata ufahamu kuhusu juhudi za Serikali katika kuhamasisha matumizi ya nishati hizo nchini ili kufikia lengo la asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.


Kongamano la Nishati Safi Expo 2026 limeandaliwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Jumuiya ya Wafanyabiashara Wanawake Tanzania (TABWA) na linafanyika katika Ukumbi wa Ubungo EACLC. 


Kongamano hilo limekuwa jukwaa muhimu linalowakutanisha wadau wa sekta ya nishati safi ya kupikia, wawekezaji na wananchi kwa lengo la kujadili mafanikio yaliyofikiwa, changamoto zilizopo na fursa za maendeleo katika sekta hiyo.


Mbali na maonesho ya teknolojia mbalimbali, kongamano hilo linaendelea kutoa fursa kwa wananchi kupata elimu kuhusu uwekezaji katika sekta ya nishati safi ya kupikia na namna wanavyoweza kushiriki katika kuharakisha matumizi ya nishati safi nchini, sambamba na kutimiza malengo ya Taifa ya kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata nishati safi na salama kwa matumizi ya kila siku.

Powered by Blogger.