MHE.SALOME: WANANCHI WANAOPITIWA NA MIUNDOMBINU YA UMEME WAUNGANISHIWE HUDUMA KWA SH. 27,000*
Na Mwandishi Wetu, Mara
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeelekeza kuwa wananchi wote ambao wamepitiwa na miundombinu ya umeme lakini bado hawajaunganishiwa huduma hiyo waunganishiwe kwa gharama ya Shilingi 27,000 tu.
Mhe. Salome ametoa kauli hiyo leo Julai 3, 2026, katika mkutano wa hadhara uliofanyika wilayani Butiama, mkoani Mara, katika ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba.
Akizungumza katika mkutano huo, Mhe. Salome amemuelekeza Meneja wa TANESCO Mkoa wa Mara pamoja na Meneja wa TANESCO Wilaya ya Butiama kubaini maeneo yote ambayo nyaya za umeme zimepita juu ya kaya za wananchi lakini bado hawajaunganishwa na huduma husika ili hatua stahiki zichukuliwe, ikiwemo kufunga transfoma katika maeneo yenye uhitaji.
Amesisitiza kuwa umeme ni nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, akieleza kuwa unachochea ukuaji wa uchumi, huboresha huduma za afya na kuinua ustawi wa wananchi, hivyo Serikali itaendelea kuhakikisha wananchi wote wanaostahili wanafikiwa na huduma hiyo.
Aidha, amesema Serikali kupitia Wizara ya Nishati imetenga zaidi ya Shilingi bilioni 38 kwa ajili ya utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Kusambaza Umeme Vitongojini katika Mkoa wa Mara. Fedha hizo zitawezesha kuendelea kusambaza umeme katika maeneo ambayo bado hayajafikiwa na hivyo kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Ameongeza kuwa, kufuatia maelekezo ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Serikali itahakikisha vitongoji 51 ambavyo havina umeme mkoani Mara vinafikiwa na nishati hiyo.
Kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia, Mhe.Salome amesema Serikali inaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Amesema katika Mkoa wa Mara tayari Serikali imesambaza majiko ya gesi zaidi ya 19,000 na majiko banifu zaidi ya 8,000 ili kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kulinda afya za wananchi na kuhifadhi mazingira.
Katika mkutano huo wa hadhara, wananchi waliwasilisha jumla ya kero sita, ambapo kero tatu zilipatiwa ufumbuzi papo hapo, huku hatua za kushughulikia kero zilizobaki zikiendelea kuchukuliwa na Serikali.



